GENN MEDIA

KANSAS COLLEGE OF NURSING

Jumatatu, 22 Juni 2015

Makongoro Nyerere Ametumwa na Nani Urais 2015?


 Hakuna kipindi ambacho CCM imeingia katika Uchaguzi Mkuu ikiwa na makundi hatarishi na pia matatizo ya kiutawala kama uchaguzi Mkuu ujao.

Ujio wa Abdulrahman Kinana kama Katibu Mkuu kwa kiasi kikubwa umekichelewesha chama kumeguka vipande vipande kabla ya Uchaguzi Mkuu ujao.

Wataalam wa kisiasa wanaendelea kujiuliza maswali mengi kuhusu hatima ya makundi na uhasama unaorutubika kila siku ndani ya CCM.

Udhaifu wa viongozi wakuu wa chama umesababisha baadhi ya wanachama kufanya watakacho kwa kukiuka kanuni, maadili na taratibu za chama mpaka kufikia hatua ya kutaka kumuondolea Rais Kikwete kofia ya Mwenyekiti wa CCM-Taifa.

Kuibuka kwa Makongoro Nyerere katika kundi la wanachama ambao wanaomba kuteuliwa kuwa wagombea Urais wa Tanzania kumeufanya uwanja wa siasa ndani ya CCM kubadilika hasa ikichukuliwa kuwa, hakuna mwanaCCM ambaye alikuwa akiongea na kusikilizwa kwa makini na wanachama wa CCM kuhusu kile kilichokua kinaendelea ndani ya CCM.

Makongoro amewashambulia vikali baadhi ya watia nia kama Edward Lowassa, Mwigulu Nchemba na Stephen Wasira kama ndiyo baadhi ya wale wanaleta maradhi ndani ya CCM pamoja na kwamba CCM bado ni chama bora nchini.

Pamoja na mambo mengine, Makongoro aliwatuhumu kwa kuja na Ilani yao ya uchaguzi badala ya kusubiri Ilani ya CCM itakayopitishwa na Mkutano Mkuu wa CCM-Taifa.

Alisema ndani ya chama hicho kumekuibuka pia genge la watu wachache ambao utajiri wao ni wa shaka na umejijenga kwa fedha chafu.

“Ndani ya chama tawala wamekuwapo ‘vibaka’ wachache… unajua kibaka ni kibaka tu hata kama kapewa gari la Serikali lina bendera ya taifa mbele atabaki kuwa kibaka tu. Hawa ndiyo wanaotuvurugia chama na hawamheshimu Mwenyekiti wa chama, Rais Jakaya Kikwete’’, Makongoro alisema.

Makongoro ameamua kuchukua jukumu la viongozi wakuu wa CCM ili kupambana na makundi yanayohatarisha uwepo wa CCM katika uwanja wa siasa.

Sauti ya Makongoro ukiichunguza kwa makini ni kama sauti ya mtu aliaye nyikani!

Kwa sauti hii, ni nani amemtuma Makongoro ili kupambana na wanachama anaowaita ni vibaka wanaosababisha baadhi ya viongozi wa CCM kuishi maisha ya kusukumwa kwa upepo wa makundi yanayomilikiwa na watoa fedha.

Je, inawezekana sauti ya Makongoro ni sauti ya viongozi wakuu wa CCM?


Makongoro atauweza mfupa uliowashinda viongozi wakuu wa CCM?.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni